Msimu wa 23 wa Kilimanjaro Marathon wazinduliwa Moshi Mjini

 

Safina Sarwatt,Kilimanjaro.


 




 

MSIMU wa 23 wa mbio za kimataifa za Kilimanjaro Premium Lager International Marathon 2025 umezinduliwa mwishoni mwa wiki katika Hoteli ya Salinero-Kilimanjaro, iliyoko Moshi, mkoani Kilimanjaro katika hafla iliyowakutanisha wadau mbalimbali wa michezo, kabla ya tukio hilo maarufu la kimataifa ambalo linatarajiwa kufanyika Februari 23, 2025.


Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu, aliyewakilishwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro Kiseo Yusuf Nzowa, alitoa pongezi kwa wadhamini, wandaaji na wadau wengine wa michezo kwa kufanya mashindano hayo kuwa endelevu, jambo ambalo limechangia kiasi kikubwa kuuweka Mkoa wa Kilimanjaro katika ramani ya dunia.

 




RC.Babu amesema kuwa mbali na kukuza afya ya watu na kukuza michezo, mbio hizo ambazo sasa ni maarufu Barani Afrika pia zinachangia kukuza uchumi wa Mkoa wa Kilimanjaro na Taifa kwa ujumla kupitia sekta ya utalii kila mwaka, kutokana na washiriki wa ngazi zote wanaokuweko mkoani Kilimanjaro kipindi chote cha mbio hizo.

 

“Tunajivunia mbio za Kilimanjaro Premium Lager International Marathon ambazo zimeendelea kuwa maarufu kila mwaka; tukio hili kwa sasa limekuwa maarufu huku likiwashirikisha zaidi ya watu 12,000 na idadi kama hiyo ya mashabiki wanaokuja mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya kulifuatilia”, alisema na kuongeza, tukio hili linawaleta pamoja watu kutoka takribani nchi 56 jambo ambalo linayafanya mashindano hayo kuwa ya kipekee ukanda wa Afrika Mashariki na ya Kati.

 




Mkuu wa Mkoa Babu alitoa rai kwa wadau wote wa michezo kushirikiana kwa Karibu na waandaaji wa mbio hizo ili ziendelee kuleta manufaa zaidi ya kiuchumi kwa Mkoa, Taifa na kwa mtu mmoja mmoja kutokana na ukweli kwamba mashindano hayo yanazidi kukua na sambamba na umaarufu wake kuendelea kukua kila mwaka.

 

"Mbio hizi huandaliwa kila mwaka na mwaka huu ni msimu wake wa 23, manafuaa yake kiuchumi yanaonekana wazi kwa jamii yote ya Watanzania, kutokana pamoja na mambo mengine kukua kwa biashara mbalimbali hususan katika mji wa Moshi; nitoe wito kwa wafanyabiashara wote wa Moshi na Mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla kuhakikisha wanazingatia ubora katika kutoa huduma zao ili kulinda heshima ya Mkoa katika nyanja za kibiashara”, alisema.

 

“Nichukue fursa hii kuwapongeza wadhamini wote wa mbio hizi wakiongozwa na mdhamini mkuu Kilimanjaro Premium Lager ambao wanadhamini mbio za kilomita, kampuni ya YAS ambao wanadhamini mbio za kilomita 21 (Yas Half Marathon) pamoja na Benki ya CRDB ambao wanadhamini mbio za kilomita 5”, alisema.

 

Aliongeza, “Napenda pia kuwaponegza wadhamini wengine ambao wanaunga mkono mbio hizo ambao ni pamoja na kampuni ya saruji ya Simba (Simba Cement), Kilimanjaro Water, TotalEnergies, kampuni ya TPC Sugar Ltd, Wasambazaji rasmi GardaWorld, CMC Automobiles, Salinero- Kilimanjaro, Kibo Palace Hotel na Keys Hotel, ambao ushiriki wao umechangia kuendelea kukua kwa mbio hizi”.









 

Akiongea katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), Khensani Mkhombo, alisema kuwa kampuni hiyo inajivunia kuwa wadhamini wa mbio hizo kwa miaka 23 iliyopita kupitia Bia ya Kilimanjaro Premium Lager na kuifanya kampuni hiyo kuwa mmoja wa wadhamini wa muda mrefu kwenye tukio moja la kimichezo hapa nchini.



 

Mkurugenzi huyo aliendelea kusisitiza ya kuwa udhamini huo pamoja na kuboresha ya watu pamoja na sekta ya michezo, pia umelenga kukuza uchumi wa Taifa kupitia sekta ya utalii kwa kuitangaza Tanzania na vivutio vyake kila msimu wa mbio hizi unapowadia.

 

“Kutokana na mbio hizi kuzidi kupata umaarufu, Mwaka huu, kamati ya maandalizi ya mbio hizi imekuja na mkakati mpya unaolenga kufanya matamasha ya utangulizi ambayo yatakayofanyika siku za mwisho wa wiki kuelekea mbio hizi, amapo matamasha hayo yataanza Ijumaa na kumalizika Jumapili ambayo ndiyo siku ya mbio hizo”, alisema na kuongeza, matamasha haya yanatarajiwa kuboresha biashara mjini Moshi.

 

Akizungumzia kuhusu zawadi zilizoandaliwa kwa msimu wa 2025, Mkhombo alisema kuwa Kilimanjaro Premium Lager imetenga jumla ya shilingi milioni 30, ambapo washidni wa kilomita 42 kwa wanaume na wanawake kila mmoja anatarajiwa kupata zawadi ay shilingi milioni 5.5, ambapo wanariadha wa Kitanzania ambao watashika nafasi ya kwanza katika mbio za kilomita 42watapata bakshishi ya 550,000/- kila mmoja.

 

Akizungumzia mafaniko mengine, Mkhombo alisema mbali na kukuza sekta ya michezo, mashindano hayo pia yameimarisha ushirikiano wa muda mrefu kati ya wadhamini, wandaaji, chama cha riadha nchini RT pamoja na jamii yote kwa ujumla.

 

Kwa upande wake, Afisa Mkuu wa Biashara YAS, Isack Nchunda alisema, "Mwaka huu tunaadhimisha na kujivunia kuwa sehemu ya udhamini wa mbio hizi maarufu Barani Afrika kwa muongo wa kumi sasa, kupitia udhamini wetu wa mbio za kilomita 21 maarufu kama Yas Half Marathon, ambapo kitengo hiki kinawaleta washiriki takribani 6,500, wakiwemo wanariadha maarufu Barani Afrika”.

 

Alisema mwaka huu, wakimbiaji na washiriki wengine wa pembeni kwa maana ya mashabiki wa mbio hizo watarajie kuona mambo mazuri kwenye mbio za kilomita 21 kutokana na uzoefu walionao wadhamini wambio hizo ambao ni Yas, ambapo alitoa rai kwa washiriki wa mbio hizo kujitokeza mapeam kuwahi nafasi zao kabla mbio hizo hazijaanza siku ya tukio hilo.

 

  

Kwa upande wao kamati ya waandaaji wa mbio hizo waliwashukuru wadhamini wakuu wa Kilimanjaro Premium Lager na YAS kwa kutenga kitita cha jumla ya shilingi milioni 53 ambazo zitatolewa kama zawadi ya Mbio za kilomita 42 na kilomita 21, pamoja na vitengo vinmgine mbalimbali.

 

Waandaaji hao pia walisema kuwa tukio hilo mwaka huu, pia linalenga kuchangia asilimia 5 ya kila malipo ya kiingilio kwa ajili ya msaada kwa Shirika la Tumaini la Maisha (TLM), msaada ambao wamesema unalenga kuwahudumia watoto wanaougua ugonjwa wa saratani ili wapate matumaini mapya baada ya kupata matibabu ya ugonjwa huo.

 

“Pesa zote ambazo zitachangwa kwa ajili ya msaada huo mwaka huu, zitaelekezwa kwenye Kituo cha Matibabu ya saratani wka watoto kilihcoko katika hospitali ya rufaa ya kanda ya KCMC (KCMC ZRH) iliyoko Moshi, mkoani Kilimanjaro”, ilsema sehemu ya taarifa ya wandaaji hao.

 

Mbio za Kimataifa za Kilimanjaro Premium Lager Marathon zinatarajiwa kufanyika Jumapili ya Februari 23, 2025, katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU), ambapo mbio hizo zimeadnaliwa na kampuni ya Kilimanjaro Marathon na kuratibiwa hapa nchini na kampuni ya Executive Solutions Limited, ambapo kampuni ya Wild Frontiers ndiyo inawajibika na matayarisho yote ya usafiri pamoja na maswala yote ya masoko yanayohusiana na tukio hilo muhimu.





 



MWISHO

Post a Comment

0 Comments